Dodoma FM

Jamii yatakiwa kutumia mitandao ya kijamii kutafuta fursa mbalimbali

25 October 2021, 11:28 am

Na; Shani Nicolous.

Wito umetolewa kwa jamii kutumia mitandao ya kijamii kutafuta fursa mbalimbali ili kujikwamua kiuchumi.

Wito huo umetolewa na katibu wa baraza la ushauri la watumiaji wa huduma za mawasiliano Tanzania Rachel Charles Elio wakati akizungumza na Taswira ya habari amesema kuwa kuna haja watu kuchangamkia fursa mbalimbali kipitia mitandao ya kijamii kuliko kuitumia vibaya.

Amesema kuwa biashara za kimtandao zinakosa uaminifu kwa kiasi kikubwa kutokana na baadhi ya watu kuitumia mitandao hiyo kutapeli watu kwa kutangaza biashara bandia na kuwaibia.

Ameongeza kuwa ili kupunguza utapeli katika mitandao kila mtu afahamu kwamba namba inayotumika kusawiliana na wahudumu wa kimtandao ni mia moja pekee na si namba za kawaida na yeyote atakayebainika akifanya vitendo vya kitapeli mtandaoni hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

Kwa upande wao baadhi ya wananchi jijini hapa wamesema kuwa mitandao ina umuhimu mkubwa ingawa ina haribiwa na watu wachache wasiojua umuhimu wake.

Mitandao ya kijamii imerahisisha shughuli nyingi za kijamii ikiwemo kutengeneza uwanda mpana wa kujifunza mambo mapya na fursa mbalimbali hivyo jamii inatakiwa kuheshimu mitandao hiyo kwa kuitumia vizuri kuliko kuharibu mila na desturi mbalimbali zilizopo nchini..