Dodoma FM

Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni saba wenye matatizo yanayo husiana na afya ya akili

11 October 2021, 12:30 pm

Na; Yussuph Hans.

Wakati Dunia ikiadhimisha Siku ya Afya ya Akili hapo jana, imeelezwa kuwa Tanzania inakadiriwa kuwa na watu milioni saba wenye matatizo yanayohusiana na afya ya akili.

Hata hivyo, sababu mbalimbali zimetajwa kusababisha matatizo ya afya ya akili ikiwemo Msongo wa Mawazo, Ugumu wa Maisha na matamanio ya kuwa na maisha bora.

Wakizungumza na Taswira ya Habari Wakazi Mkoani Dodoma wamekiri kuwa ugumu wa maisha na matamanio ya kuwa na maisha bora ni sababu ya kuwa na msongo wa mawazo huku wakitumia njia mbalimbali kuhakikisha wanajikwamua katika changamoto hizo.

Aidha wameshauri jamii kuhakikisha inakuwa na mawazo chanya pamoja na fikra za kuwa na uchumi bora ili kukwepa msongo wa mawazo ambao baadhi ya muda husababisha watu kuwa warahibu wa vileo wakiamini kufanya hivyo ni njia ya kuwepa msongo wa mawazo.

Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) zinaonyesha kufikia mwaka 2020 watu bilioni moja walikuwa wanaishi na magonjwa ya akili huku wengi walio katika hatari ni wenye umri kuanzia miaka 15 hadi 39.