Dodoma FM

Serikali yapiga marufuku watoto wadogo kutumikishwa kuchunga mifugo

7 September 2021, 2:32 pm

Na;Yussuph Hans.

Serikali Nchini imepiga marufuku Watoto wadogo kutumikishwa kuchunga mifugo kwani wanahitajika kwenda Shule pamoja na kwamba hawamudu kundi kubwa la Mifugo.

Hayo yamebanishwa leo na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Kassim Majaliwa katika Mkutano wa wadau wa Sekta ya Mifugo uliofanyika Jijini Dar Es Salam.

Mh Majaliwa amesema kuwa licha ya baadhi ya Tamaduni kupenda kufanya hivyo, ni lazima wabadilike ili kuepusha migogoro kati ya wakulima na wafugaji pamoja na kuipa muelekeo mzuri katika sekta hiyo hapa nchini.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuboresha sekta hiyo huku akiwataka wadau kuwa wabunifu ili kupata mafanikio.

Aidha ameziagiza mamlaka za serikali za mitaa kutenga asilimia 15 ya mapato yatokanayo na mifugo pamoja na viongozi wa serikali kuwa karibu na wafugaji ili kuimarisha uwekezaji.

Mkutano wa wadau wa Sekta ya Mifugo umefunguliwa leo rasmi jijini dar es salam na kuwatanisha viongozi kutoka taasisi mbalimbali huku kauli mbiu ikiwa ni “kufikia tanzania ya viwanda 2025 ushiriki wa sekta binafsi katika sekta ya mifugo ni nguzo muhimu kuinua uchumi na kuongeza ajira”.