Dodoma FM

Kwa mujibu wa tafiti zilizo fanywa 2018 asilimia 31.8 ya watoto Nchini wakabiliwa kuwa na udumavu

6 August 2021, 9:59 am

Na;Mindi Joseph .

Ikiwa ni Maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji Maziwa ya mama Duniani asilimia 31.8 ya watoto nchini wametajwa kuwa na udumavu kwa mujibu wa utafiti wa hali ya lishe mwaka 2018.

Hayo yamebainishwa leo na Mratibu wa Lishe ya mama mtoto na Kijana Balehe kutoka Wizara ya afya Bi. Tufingene Malambugi katika semina ya waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dodoma ambapo amesema katika Mkoa wa Dodoma asilimia 37.2 ya watoto wamedumaa.

Ameongeza kuwa kudumaa kwa watoto inawaweka katika hatari ya kukumbwa na ukuaji duni wa kimwili na kiakili na kuchangaia maendeleo kuwa duni shuleni pamoja na kuwa na uwezekano wa kupatwa na magonjwa mbalimbali.

Akizungumza katika ufunguzi wa semina hiyo Kaimu Mkurungezi huduma za lishe Grace Moshi amesema Maadhimisho haya yanafanyika ulimwenguni kote na kitaifa yamezinduliwa wilayani songwe Augosti Mosi.

Kwa upande wake Ruth Mkopi Afisa tafiti mwandamizi Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania amesema unyonyeshaji ni muhimu kwani unaweza kuzuia vifo vya watoto duniani kote kwani watoto wakinyonyeshwa vizuri inaweza kuzuia vifo vya watoto asilimia 12 chini ya miaka 5.

Maadhimisho ya Wiki ya unyonyeshaji mwaka huu yanaenda sambamba na kauli mbiu isemayo “Kulinda unyonyeshaji wa maziwa ya mamani jukumu letu sote”