Dodoma FM

Matumizi makubwa ya nishati ya mkaa na kuni yatajwa kuwa chanzo kikuu cha uharibifu wa mazingira Nchini

1 July 2021, 11:07 am

Na;Mindi Joseph .

Matumizi ya kuni na Mkaa huchangia miti mingi kukatwa na kusababisha uharibifu wa mazingira.

Kwa mujibu wa ripoti ya Hali ya Upatikanaji wa Nishati iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu mwaka 2016 inaonyesha kuwa asilimia 88.2 ya kaya za jiji la Dar es Salaam zinatumia mkaa kama nishati huku asilimia 94.3 ya kaya za Simiyu zinatumia kuni, jambo linaloashiria kuchangia uharibifu wa mazingira na kuongezeka kwa hewa ukaa.

Taswira ya Habari imezungumza na Abraham Biamungu afisa mwekezaji mwandamizi UNDP amesema katika kupungumza matumizi ya mkaa kwa majiji makubwa nchini wamejipanga kuhakikisha wanatoa elimu zaidi ya matumizi ya nishati mbadala ambayo ni rafiki kwa mazingira.

Naye Abas Kitogo Afisa Miradi ya Mabadiliko Tabia Nchi kutoka shirika la umoja wa mataifa la maendeleo amesema uelewa mkubwa unahitajika katika jamii hususani matumizi ya nishati mbadala ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo yanachochea kuendelea kuongezeka kwa hewa ukaa.

Asilimia 70 hadi 80 ya miti mikubwa inayokatwa nchini hutumika kutengenza mkaa, hivyo kuna kila sababu kwa nchi kutoa elimu zaidi ya matumizi ya nishati mbadala ili kupunguza matumizi ya mkaa.