Dodoma FM

wanawake Dodoma wamshukuru rais Samia.

23 June 2021, 11:34 am

Na; Benard Filbert

Baadhi ya wanawake jijini Dodoma wamemshukuru rais Mh.Samia Suluhu Hassan kufuatia ongezeko la idadi ya wanawake ambao wameteuliwa hivi karibuni katika nafasi ya wakuu wa Wilaya nchini.
Wakizungumza na taswira ya habari wanawake hao wamesema kitendo cha rais kuwateua wanawake kimeleta picha nzuri katika jamii tofauti na ilivyokuwa awali.
Wamesema uteuzi huo utaendelea kubadilisha mtazamo katika jamii na kuiaminisha kuwa mwanamke anaweza.

Cesilia Shirima ni mkurugenzi kutoka Shirika lisilo la kiserikali la Young And Alive Initiative ambalo limekuwa likijihusisha na masula ya vijana na wanawake ameiambia taswira ya habari kuwa kuongezeka kwa wanawake katika nafasi ya wakuu wa Wilaya inajenga picha nzuri kwa jamii.
Ameongeza kuwa awali kulikuwepo na mfumo dume katika uongozi nchini hivyo jamii iwaangalie wanawake katika nafasi zote na sio jinsia zao.

Hivi karibuni rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Samia Suluhu Hassan alifanya uteuzi wa wakuu wapya wa Wilaya huku ikionesha 56 ni wapya na wa zamani 83 huku wanaume wakiwa 95 na wanawake 44 sawa na asilimia 31.6 tofauti na hapo awali.