Dodoma FM

Wakuu wa mikoa wapya wametakiwa kusimamia ipasavyo huduma kwa wananchi

21 June 2021, 2:05 pm

Na; Yussuph Hans.

Wakuu wa Mikoa walioapishwa hii leo wametakiwa kuhakikisha wanasimamia ipasavyo huduma kwa wananchi katika maeneo wanayoenda kuyatumikia.

Wito huo umetolewa na waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Kassim Majaliwa hii leo wakati rais Rais Mh.Samia Suluhu Hassan akiwaapisha Balozi Batilda Buriani Mkuu wa Mkoa wa Tabora na Zuwena Omari kuwa Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga baada ya uteuzi wao uliofanyika June 11, 2021.

Mh.Majaliwa amesema kuwa lazima huduma kwa wanachi zitolewe kwa kiwango bora na kuleta matokeo chanya yatakayowafanya watanzania kujivunia Serikali yao.

Ameongeza kuwa ni muhimu kuzingatia usimamizi wa shughuli za Serikali na kuwa na mipango mizuri ili kuwaletea wananchi maendeleo.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Mh.Ummy Mwalimu amesisitiza juu ya maagizo ya Rais Mh.Samia Suluhu Hassan kuhakikisha halmashauri zinakusanya fedha kwa ajili ya kutatua changamoto za mahali husika.

Zoezi la kuwaapisha viongozi hao limefanyika Ikulu Chamwino Jijini Dodoma hii leo.