Dodoma FM

Waziri Awesso afanya ziara ya kukagua miradi ya maji wilaya ya Kongwa

4 June 2021, 1:23 pm

Na; Selemani Juma.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso ameagiza kuondolewa katika wizara hiyo mhandisi wa maji wa Wakala wa Maji Vijijini (Ruwasa) Wilaya ya Hanang, Herbert Kijazi baada ya kuisababishia hasara Serikali ya Shilingi milion 609.

Hatua ya hiyo imekuja baada ya Waziri Awesso kufanya Ziara ya kukagua Miradi ya maji katika Wilaya ya kongwa ambapo amesema kwa mujibu wa taarifa iliyoanishwa katika ripoti ya maabara juu ya Mradi wa maji mkoka unaonesha maji hayo sio salama kwa matumizi ya Binadamu huku mhandisi huyo akiidhinisha utekelezaji wa mradi huo.

Vilevile Waziri wa Maji Jumaa Awesso amewataka Mhandisi wa wakala ya Maji Vijijini RUWASA mkoa wa Dodoma Godfrey Mbabaye na meneja wa Wilaya ya Kongwa,Kaitaba Rugakingira kujieleza kwake kwa nini wasifukuzwe kazi kwa kutaka kusababisha hasara nyingine baada ya kumweleza kuwa wanahitaji Sh360 milioni ili kukarabati mradi wa maji mkoka .

Aidha Waziri Awesso amewahakikishia wakazi wa kongwa kuwa ifikapo mwezi wa nane wataanza kupata maji baridi ikiwa ni utekelezaji wa kuhakikisha wananchi wa tanzania watumia maji safi na salama na yenye Ubora.

Pamoja na hayo ,Waziri Awesso amefanya ziara ya kukagua mradi wa uchimbaji wa maji katika Vijiji vya Ijaka,Ibwanga pamoja na mradi wa mji wa kongwa ikiwa ni sehemu ya utekelezaji na kufanikisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa wilaya ya kongwa.