Dodoma FM

TMA yakutana na wadau wa sekta ya kilimo na mifugo jijini Dodoma

1 June 2021, 11:53 am

Na ;Victor Chigwada.

Wadau wa sekta ya kilimo na mifugo wameelezea namna watakavyotumia utabiri wa hali ya hewa kufanikisha kazi zao kwa ufanisi zaidi.

Wakizungumza katika warsha iliyofanyika katika chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo iliyo andaliwa na mamlaka ya hali ya hewa Tanzania TMA ikiwahusisha wadau wa sekta ya kilimo wamesema watafanyia kazi elimu waliyoipata na wataifikisha kwa wakulima na wafugaji ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria katika warsha hiyo.

Nae kaimu mkurugenzi mkuu wa TMA Dkt.Ladislaus Chang’a ameishukuru mamlaka ya hali ya hewa TMA kwa kuwawezesha kutimiza azma yao ya kuwakutanisha na maafisa mifugo pamoja na maafisa ugani.

Dr.Chang’a amesema anaamini warsha hiyo imewasaidia washiriki kujenga uelewa, na kuwa TMA imefahamu maeneo mengine ya kwenda kuboresha zaidi ili kuendelea kutoa huduma ya utabiri wa hali ya hewa kwa manufaa ya sekta hizo.

Wakulima na wafugaji wengi nchini wamekuwa hawana elimu ya kutosha juu ya namna ya kutumia utabiri wa hali ya hewa kufanya shughuli zao kwa tija, ambapo TMA imeendelea kutoa mafunzo mbalimbali ili kuhakikisha utabiri huo unawanufaisha.