Dodoma FM

Rais Samia: sheria ya PF3 iangaliwe upya

18 May 2021, 1:20 pm

Na; Benard Filbert

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.Samia Suluh Hassan ameliagiza jeshi la Polisi nchini kuangalia upya sheria inayomtaka mgonjwa aliyepata ajali kutokutibiwa bila kuwa na fomu namba tatu ya Polisi(PF3) kwani imekuwa ikisababisha watu wengi kupoteza maisha kutokana na utaratibu wa upatikanaji wake.

Rais Samia amesema hayo leo jijini Dar Es Salaam wakati akizindua kiwanda cha Polisi cha ushonaji kilichopo eneo la Kurasini.

Amesema kuwa sheria hiyo hairuhusu mtu aliyepata ajali kupatiwa matibabu bila kuwa na fomu hiyo jambo ambalo linasababisha idadi kubwa ya watu kupoteza maisha hivyo ni vyema akapatiwa matibabu na baadaye utaratibu mwingine ufuatwe.

Taswira ya habari imezungumza na baadhi ya wananchi jijini Dodoma ambao wamesema ni vyema jeshi la polisi likaangalia vizuri sheria hiyo kwani watu wengi wanapoteza maisha kutokana na utaratibu mgumu wa upatikanaji wa PF3.

PF3 ni fomu namba tatu ya polisi ambayo daktari hujaza maelezo ya mgonjwa kwa ajili ya mchakato wa kesi hapo baadaye..