Dodoma FM

Wazazi kata ya makanda wataka matokeo chanya kwa wanafunzi

12 May 2021, 1:00 pm

Na; Victor Chigwada

Kutokana na matokeo yasiyokuwa ya kuridhisha kwa wanafunzi wa shule za sekondari katika Kata ya Makanda wazazi wametaja kilichosababisha hali hiyo ni kuwepo kwa kambi za kitarafa.

Baadhi ya wazazi hao wakizungumza na taswira ya habari wamesema wameamua kuwa ni bora wanafunzi kubaki katika shule zao ili kujisomea kwa bidii kuliko kupangiwa mzunguko wa kambi ambao umeleta matokeo hasi tofauti na awali

Mwenyekiti wa kijiji cha Chonde Bw.Richadi  Ndahani amesema kutokana na mzunguko huo wa kitarafa kwa wanafumzi umeporomosha matokeo kutoka nafasi ya kwanza kiwilaya mpaka nafasi ya kumi na moja, hivyo wazazi wamependekeza kambi zisimamiwe katika shule husika.

Naye Diwani wa Kata ya Makanda Bw.Boniface Nyamuda  amekiri kuwa mwaka jana zilifanyika kambi za kitarafa hivyo kuchangia mzunguko mkubwa na kupelekea matokeo hasi lakini bado wanamatarajio ya kufanya vizuri kama ilivyokuwa kwa hapo awali tofauti na mwaka jana.

Mwanafunzi anatakiwa kukaa shuleni siku 194 kwa mwaka lakini kwa mwaka jana 2020 zilipungua kutokana na shule kufungwa wakati wa mlipuko wa janga la corona hivyo ziliihitajika jitihada binafsi za shule  au Kata kufidia muda huo waliokaa nyumbani .