Dodoma FM

Wananchi Makulu waomba bodaboda wanao fanya uhalifu wachukuliwe sheria kali

6 May 2021, 7:59 am

Na; Joan Msangi.

Kufuatia baadhi ya watu wanaoendesha pikipiki maarufu kama bodaboda kudaiwa kujihusisha na uhalifu , wananchi katika Kata ya Makulu jijini  Dodoma wameiomba Serikali kuwachukulia hatua kali za kisheria watakaobainika.

Wakizungumza na Dodoma fm wananchi hao wamesema nyakati za usiku kumekuwa na matukio ya uporaji na ukabaji ambao umekua ukiwakosesha amani ambapo wametoa wito kwa vyombo husika kufanya ukaguzi wa leseni pamoja na vyombo vinavyotumika ili kukabiliana na tatizo hilo.

Nao baadhi ya madereva boda boda wamesema kuna baadhi yao wasio waaminifu ambao wamekuwa wakifanya vitendo hivyo nyakati za usiku hivyo kuwaletea sifa mbaya madereva wote.

Bw.Juma Arafat ambaye ni mtendaji wa Kata ya Makulu amesema Serikali bado inaendelea kukabiliana na changamoto hiyo kupitia vyombo vyake  lakini ni vyema wananchi wakawa na utaratibu wa kuchukua usafiri kwenye vituo vinavyotambulika.