Dodoma FM

Uongozi wa secondary ya Hombolo bwawani wakanusha taarifa ya kuadhibu wanafunzi kupita kiasi

4 May 2021, 9:44 am

Na; Benard Filbert

Uongozi wa shule ya secondary Hombolo bwawani  jijini Dodoma umekanusha  taarifa zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii kuhusu wanafunzi wa kidato cha tano kuadhibiwa hadi kufikia hatua za kulazwa hospitali kutokana na uharibifu wa mali za shule.

Akizungumza na taswira ya habari mwalimu mkuu wa shule hiyo Bw. Joseph Kapalambi amesema ni kweli kuna baadhi ya wanafunzi wa kidato cha tano  shuleni hapo walifanya uharibifu wa bustani ya shule lakini kuna baadhi ya  vyombo vya habari viliripoti  tofauti  tukio hilo .

Amesema kitendo kilichofanywa na wanafunzi hao kaharibu bustani ya shule ni utovu wa nidhamu pamoja na uvivu wa kutokufanya kazi hivyo wamevunja sheria za shule.

Naye diwani wa kata ya Hombolo bwawani Bw. Ased Ndajilo amesema taarifa za awali ambazo ziliripotiwa kwenye moja ya chombo cha habari hazikuwa sahihi kwani hakuna mwanafunzi aliye lazwa kutokana na kupewa adhabu ya uharibifu wa bustani ya shule.

Hivi karibuni kupitia mitandao ya kijamii zilisambaa taarifa zikieleza wanafunzi wa kidato cha tano shule ya sekondari Hombolo bwawani wameadhibiwa   kupita kiasi na walimu wote wa shule hiyo kutokana na kuharibu shamba la bamia la mwalimu wa shule hiyo taarifa ambazo hazikuwa na ukweli ndani yake.