Dodoma FM

Ujenzi wa Bomba la Mafuta utachangia kukuza uchumi wa Tanzania

13 April 2021, 11:31 am

Na ;Benard Filbert.

Kuanza kwa ujenzi wa mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima Nchini Uganda hadi Tanga Tanzania mwishoni mwa mwezi huu kunatarajiwa kufungua fursa za kiuchumi kwa watanzania wengi.

Hayo yamebainishwa na mchambuzi wa masuala ya kisiasa na kijamii Jawadu Mohamed wakati akizungumza na taswira ya habari kuhusu fursa za kiuchumi ambazo watanzania watanufaika nazo wakati wa ujenzi huo.

Jawadu ameiambia taswira ya habari kuwa ujenzi huo utachangia kukuwa kwa uchumi wa nchi huku ikikadiriwa kuwa Tanzania itakuwa ikipata zaidi ya dola milioni 2 kwa siku.

Ameongeza pia maeneo ambayo bomba hilo litapita kutakuwa na mwamko wa kibiashara hivyo kuongeza ajira kwa wananchi.

Kwa upande wake profesa Enock Wiketie kutoka chuo kikuu cha Iringa amesema kujengwa kwa bomba hilo kutachangia kutoa ajira za moja kwa moja na za muda mfupi kwa Watanzania.

Hivi karibuni rais wa Tanzania Mh.Samia Suluhu Hassan na mwenzake wa Uganda Yoweri Museveni wamesaini rasmi mkataba wa utekelezaji wa mradi huo wa bomba la mafuta ghafi kutoka Magharibi mwa Uganda hadi bandari ya Tanga Tanzania.