Dodoma FM

Wanawake na nafasi za juu katika uongozi

12 April 2021, 9:13 am

Na; Mariam Kasawa.

Tanzania ni miongoni mwa Nchi ambayo imekuwa ikiwapa kipaumbele wanawake hasa katika nyaja ya uongozi.

Akizungumza leo katika kipindi cha Dodoma live Bi. Gloria Mafole wakili mchambuzi wa sera kutoka katika Jumuiya ya kikristo Tanzania amsema wanawake wamekuwa wakipewa nafasi ya kuongoza sekta mbalimbali na kulingana na utendaji kazi wao wamekuwa hawaliangushi Taifa katika nafasi wanazo pewa kwani huwa wanazitendea haki nafasi hizo.

Akitolea mfano uongozi wa awamu ya nne wa Rais Jakaya Kikwete Bi. Mafole amesema Bunge liliongozwa na spika mwanamke Anna Makinda ambae aliongoza vizuri Bunge kwani hadi anamaliza muda wake hakukuwahi kutokea vurugu yoyote Bungeni licha ya kuwa bunge lilikuwa na upinzani mkubwa kipindi hicho.

Amesema Si Mama Anna Makinda pekee bali wanawake wameshika uongozi katika nyanja mbalimbali ndani ya Taifa hili mfano katika nafasi ya baraza la mawaziri wapo pia wanawake ambao wanafanya vema zaidi na kuzipa jamii nyingi za Nchi yetu zilizo kuwa zikiamini zaidi mfumo dume kuangalia kwa upana zaidi na kuamini kuwa mwanamke anaweza kuongoza pale anapo pewa nafasi.

Mnamo tarehe 17 Machi 2021 majira ya saa tano usiku Nchi ya Tanzania iligubigwa na kiza kinene baada ya aliye kuwa makamu wa Rais Mama Samia Suluhu kutangaza kuwa Rais John Pombe Magufuli ameaga dunia , hali hii ilifanya wananchi wengi kuingia woga, majonzi na kutumia muda mwingi kuwaza itakuwaje na nani atakuja baada ya hapa.

kulingana na katiba na sheria ya Nchi hii baada ya Rais kufariki anae chukua madaraka ni kiongozi anae mfata , Mama Samia Suluhu Hassan aliapishwa kuwa Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo kuleta Tumaini tena kwa Watanzania ambao walikuwa hawaelewi kuwa baada ya msiba huu itakuwaje .

Mama Samia Suluhu licha ya kuliongoza Taifa kwa kipindi hiki kifupi amekuwa kiongozi mahiri na shupavu amedhihirisha ukomavu wake katika uongozi na pia ametumia nafasi yake kama mama kuliongoza Taifa vema.