Dodoma FM

Waziri jafo aipa machinjio ya kizota miezi sita kujenga mfumo wa kutibu majitaka

8 April 2021, 10:00 am

Na ; Mariam Kasawa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo ameupa uongozi wa machinjio ya kisasa ya Kizota jijini Dodoma miezi sita kurekebisha changamoto ya utiririshaji wa majitaka ovyo.

Jafo ametoa agizo hilo leo Aprili 8, 2021 alipofanya ziara ya kikazi katika machinjo hiyo kwa ajili ya kukagua udhibiti wa majitaka na utunzaji wa mazingira kwa ujumla.

Amesema kuwa kila kiwanda lazima kiwe na mpango wa namna ya kuyatibu majitaka na kudhibiti utiririshaji wake kuepusha yasiende kwenye makazi ya watu na kusababisha madhara ya kiafya.

Amesema “Nafahamu machinjio hii ni miongoni mwa machinjo kubwa na ina soko kubwa katika nchi za Mashariki ya Kati wananunua nyama nami nimekuja hapa kujiridhisha kuhusu suala zima la utiririshaji wa majitaka .

Alimuelekeza Meneja wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC) Kanda ya Kati Flanklin Rwezimula kufuatilia kazi ya kuhakikisha machinjio hiyo inatengeneza mfumo wa kutibu majitaka haraka.